Monday 11 April 2011

TAARIFA YA DHARURA TOKA CHAMA CHA WANASHERIA TANGANYIKA

Tarehe 9 Aprili, 2011

DAR ES SALAAM

Uundwaji wa Chama cha Wanasheria cha Tanzania Bara na Majukumu yake

Chama cha Wanasheria cha Tanzania Bara (“TLS”) ni Taasisi ya Wanasheria wa

Tanzania Bara iliyoanzishwa kwa Sheria ya Chama cha Wanasheria cha Tanganyika,

Sura ya 307 Toleo la 2002. Kwa mujibu wa Sheria hii, Chama kina, pamoja na mambo

mengine, jukumu la kuisaidia Serikali katika mashauri yanayohusu utungaji wa sheria

na utekelezaji na matumizi ya sheria, na pia kulinda na kusaidia umma katika masuala

yote yanayohusika na kadhia za sheria.



Chama cha Wanasheria kinatoa taarifa hii kwa mujibu wa mamlaka mahsusi ya sheria .



Mazingira ya Muswada wa Sheria ya Marejeo ya Katiba, 2011

Tarehe 11 Machi, Muswada wa Sheria ya Marejeo ya Katiba, 2011 (kwa kifupi

“Muswada”) ulitangazwa katika Gazeti la Serikali la Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Toleo Namba 1 Jarida Na.2. Chama kilipata nakala ya Muswada huo Jumanne, tarehe 30

Machi, na kilisambaza hizo taarifa kwa wanachama wake siku ya Alhamisi tarehe 31

Machi ili kupata maoni yao. Siku ya Jumamosi tarehe 2 Aprili, Chama cha Wakufunzi wa

Chuo cha Dar es Salaam (UDASA) waliendesha mjadala wazi kuhusu Muswada, mjadala

ambao uliripotiwa kwa mapana katika vyombo vya habari. Siku ya Jumanne, tarehe 5

Aprili, Chama chetu kilialikwa kupitia Kurugenzi ya Kamati za Bunge (“Kurugenzi”)

kushiriki katika mjadala juu ya Muswada ambao ulipangwa kujadiliwa na Kamati ya

Katiba, Sheria na Utawala ya Bunge (kwa kifupi “Kamati”) tarehe 7 Aprili Dodoma, kama

ilivyopangwa awali. Mnamo mwisho wa siku hiyo Chama chetu kiliulizia maendeleo

kuhusu mijadala bayana, na kikahabarishwa kwamba sasa sehemu mpya tatu (3)

zimetajwa kwa ajili ya mijadala bayana, yaani Dodoma, Dar es Salaam na Zanzibar;

aidha taarifa tulizopata ni kwamba mijadala itafanyika tarehe 7 na 8 Aprili, na ikibidi

tarehe 9 Aprili. Kutokana na uthibitisho huu,Chama chetu kikaahidi kushiriki kikao cha

Dar es Salaam.

Jumanne tarehe 5 Aprili Muswada uliwakilishwa Bunge ni kwa Hati ya Dharura isomwe

mara ya kwanza. Tarehe 7 Aprili, Rais wa Chama chetu aliipelekea Kamati - kwa

maandishi - maoni na mapendekezo ya wanachama wa Chama cha TLS kuhusu

Muswada. Tarehe 8 Aprili, Rais wa Chama cha TLS alitoa mapendekezo kwa mdomo.

Baada ya kushiriki katika mijadala ya umma, Chama kilitiisha mdahalo kuhusu

Muswada kwa wanachama ili kuhakikisha mawazo ya wanachama wengi iwezekanavyo

yanakusanywa kuthibitisha msimamo wa wengi katika C hama.


Hoja na Maoni

UTANGULIZI

Kwa kuwa Chama cha TLS kimejizatiti kwa dhati kuimarisha na kuendeleza

utawala wa sheria nchini Tanzania, kwa kujua kwamba sheria inapozingatiwa

ipasavyo, utawala wa sheria huwalinda wananchi dhidi ya matumizi ya kibabe ya

mamlaka ya Serikali; kwa kuwa tunaafiki dhana kwamba sheria zote lazima

zitungwe kwa shabaha ya kuenzi Utawala wa Sheria, utawala bora na nyanja ya

demokrasia ambayo imejengewa misingi imara katika falsafa ya haki ya nchi yetu

na ambayo inashabihiana na viwango vya kimataifa na vyenye ubora maridhawa;

kwa kuwa Chama kinaamini kwa dhati kwamba hatima na mchakato mzima

kuhusu marejeo na utungaji wa Katiba mpya unapaswa kupata uhalali muafaka

kwa njia ya ushirikishwaji wa wananchi; na kwa kusisitiza kwamba haki haitakiwi

tu ifanyike, bali pia ionekane kwamba inafanyika, Chama kinaeleza msimamo

wake mintarafu ya Muswada kama ifuatavyo:

1. Kuhusu lugha ya Muswada: Chama kinapendekeza kwa msisitizo kwamba

Muswada utangazwe katika lugha ya Kiswahili, kwa kuzingatia dhana ya haki

kupatikana (jambo ambalo linamaanisha mtu wa kawaida kupata nakala na

uelewa) kwa Watanzania wote (wanaoishi vijijini na mijini, wananchi wa

kawaida, wenye mapato ya kati na wa matabaka ya juu), ikiwa ni sambamba na

lugha inayotambulika ya toleo rasmi la Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya

Tanzania, 1977 (kwa kifupi “Katiba”);

2. Kuhusu jina la Muswada: Chama kinashauri kwa dhati kwamba jina la

Muswada lisomeke ‘Muswada wa Kutunga Katiba Mpya, 011’ ili kuonyesha

dhahiri nia ya wananchi (kwamba wanataka Katiba mpya, siyo marekebisho

yake) katika mchakato mzima;

3. Kuhusu maelezo ya awali la Muswada: Chama kinapendekeza kwamba tamko

la awali lirekebishwe na lioneshe wazi madhumuni: MUSWADA wa Sheria

itakayoweka mfumo wa kutunga/kuweka Katiba mpya inayokidhi vigezo

vinavyokubalika kimataifa vya demokrasia na utawala bora’;

4. Kuhusu ukomo wa Katiba na utungaji wa rasimu ya Katiba mpya: Chama

kinatoa tahadhari kwamba Katiba ya sasa haisemi lolote kuhusu ukomo wa

Katiba na utungaji wa katiba mpya; kwa mujibu wa Ibara ya 98, ni utaratibu

pekee unaotajwa wa kufanya marekebisho. Kutokuwepo kwa vipengele vya suala

hili kutafanya michakato yoyote ya kuunda Katiba mpya kuwa batili.

Hivyo basi kama jambo la lazima, Chama kinapendekeza kwa dhati yafanywe

marekebisho ya Katiba, kuwekwe vipengele vitakavyoruhusu utaratibu wa ukomo

wa Katiba iliyopo na utungaji wa Katiba mpya.

5. Kuhusu kifungu cha 5 cha Muswada - Uundwaji wa Tume: Chama kinashauri

kwa dhati kwamba Tume iundwe moja kwa moja na Sheria hii. Lugha

inayotumika katika Muswada inakasimu kwa Rais wa Jamhuri ya Tanzania

mamlaka ya kuunda Tume ambapo Rais atakuwa na uhuru wa utendaji. Aidha

Rais analazimika kuunda Tume hiyo baada ya tarehe 1 Juni 2011 (tarehe ambapo

sheria hii itaanza kutumika), lakini hakuna kikomo kinachotajwa cha jukumu

hili.

Ili kurekebisha kasoro hizi, kifungu hiki kisomeke, “Tume ya Katiba inaundwa

kwa Sheria hii.”

6. Kuhusu kifungu cha 6 cha Muswada - Uteuzi wa wajumbe wa Tume: Chama

kinatoa maoni na mapendekezo yafuatayo:

*Uwakilishi katika Tume:

Muswada unapendekeza Tume iwe na

uwakilishi wa Tanzania Bara na Visiwani kwa idadi sawa. Lakini kifungu

hiki hakizingatii hata kidogo tofauti ya ukubwa wa idadi ya watu na

kwamba Katiba ya Muungano inahusika na Zanzibar pale tu masuala ya

Muungano yanapotajwa. Hivyo basi, ili kuhakikisha kuna uwiano stahiki

katika Tume (yaani unaozingatia sura halisi ya mambo), idadi ya

wajumbe kutoka Tanzania Bara na kutoka Visiwani izingatie idadi ya

watu.

*Muundo wa Tume:

Tume iwe Jopo la Wataalamu watakaoteuliwa
kutoka mchanganyiko wa kada za taaluma, mashirika na jumuiya
mbalimbali kwa kuzingatia jinsia, dini na ngazi za utaalamu. Aidha kif.

6(2)(e) kinampa Rais mamlaka ya kuteua kwa hiari yake wajumbe wa

Tume wasiokuwa katika makundi ya watu waliotajwa katika fasili (a)

hadi (d)- jambo ambalo linaweka mwanya wa matumizi mabaya ya

madaraka.


7. Kuhusu Kifungu cha 8 cha Muswada - Hadidu za Rejea (kwa kifupi

“hadidu”) za Tume: kwa ajili ya uwazi na uwajibikaji, Chama kinapendekeza

kwamba hadidu ziandikwe na chombo huru na ziidhinishwe na Bunge la

Tanzania, badala ya Rais.

8. Kuhusu Kifung cha 14 cha Muswada – Gharama za Tume: Muswada

unadhihirisha dhamira ya Serikali kwamba matumizi ya Tume yatalipwa kutoka

Mfuko Mkuu wa Serikali. Chama kinapendekeza kwa msisitizo kwamba kuwe na

mfumo wazi, bayana na wa uwajibikaji katika kuidhinisha na kutoa taarifa za

matumizi.

9. Kuhusu Kifung cha 16 cha Muswada – Kutoa taarifa kwa Rais: ili pawe na

mfumo wazi na bayana, Chama kinapendekeza kwamba Taarifa ya Tume iweze

kupatikana kwa umma, yaani wananchi waione na waruhusiwe kutoa maoni yao

juu yake, hata kama taarifa inapelekwa kwa Rais.

10. Utekelezaji: ili kuhakikisha kwamba Watanzania hawaachwi nje ya mchakato

huu, Chama kinapendekeza kwa msisitizo kwamba shughuli ya Tume – kwa

mtizamo wa kawaida – zifanyike mikoa yote 26 ya Tanzania, na siyo katika

baadhi tu ya mikoa, kama msimamo ulivyojitokeza kwenye mijadala bayana

iliyoendeshwa na Kamati ya Bunge.

11. Kuhusu vipengele visivyoruhusiwa kuguswa – Kifungu cha 9 (2) na 20 (1):

Muswada unafanya vipengele vya msingi vinavyohusu ibara za msingi za Katiba

visiguswe. Kwa mfano, kif. 9 (2) kinataka mambo ya Muungano na suala la ofisi

ya Rais, mambo yote mawili ambayo yaliyowekwa na Ka tiba, yasiguswe. Kif. 20

(1) kinakinzana na Ibara 26(2) ya Katiba ambayo inalinda haki ya mwananchi

kupinga uhalali wa kikatiba wa sheria za nchi. Kuviacha vifungu vibaki pia ni

kukiuka utekelezaji wa Utawala wa Sheria.


12. Kuhusu kasoro za uchapishaji zimebainika, lazima ziepukwe kwa

uangalifu: Usahihi wa Muswada unategemea uandishi na rejea sahihi. Kwa

mfano, kif. 19 kinatakiwa kurejea kif. 18 na siyo kif.19; na kif. 20 (3) kirejee kif.

20(2) na siyo kif. 20 (1). Athari ya hili la pili, kwa mfano, ni kumtwika tuhuma ya

jinai mtu yeyote anayeamua kufungua shauri mahakama ni kupinga Sheria hii –

jambo ambalo ni kinyume na Katiba, na ni ukiukwaji wa haki na wajibu wa

msingi.

13. Kuhusu Kifungu cha 21 cha Muswada - Kutangazwa Baraza la Kutunga

Katiba: Muswada unatamka kwamba Rais ana mamlaka ya kuunda Baraza la

Kutunga Katiba na kwamba anaweza kutamka Bunge lijigeuze kuwa Baraza la

Kutunga Katiba.


Chama kinapendekeza kwamba Rais asiwe na mamlaka ya kuligeuza Bunge

kuwa Baraza la Kutunga Katiba, na kwamba muundo wa Baraza uamuliwe na

wananchi watakaoteuliwa kutoka kada mbalimbali (yaani taaluma na uzoefu,

mashirika, taasisi za kidini na makundi mbalimbali).

14. Kuhusu Kifungu 26 cha Muswada – Kusimamia kura ya maoni

(referendum): inaonekana kwamba Tume ya Taifa ya Uchaguzi si mahala pake

kuratibu suala la uhalalishaji wa Katiba. Chama kinapendekeza kwamba taasisi

za jamii, vyama vya siasa na watu binafsi na makundi mengine waruhusiwe

kushiriki kwa uhuru uelimishaji wa umma kuhusu upigaji wa kura ya maoni.

Hatimaye Tume ya Katiba idhibiti uenendeshaji wa upigaji kura ya maoni.

15. Kuhusu sehemu ya VI – Uhalalishaji wa Katiba : Chama kinapendekeza

kwamba mchakato wa uhalalishaji uendeshwe na Tume, siyo Tume ya Taifa ya

Uchaguzi, kwa kuwa imeundwa na Katiba.

Mpango wa Chama wa Hitimisho:

a. Chama kinashauri kwa dhati kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano ya

Tanzania, Mheshimiwa Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, aiondoe Hati ya Dharura

iliyoambatanishwa na Muswada uliowasilishwa Bungeni. Kwa ushauri wa Chama

Muswada ufuate utaratibu wa kawaida ili Wabunge na umma wote upate fursa

ya kutosha kujadili na kutoa maoni kuhusu Muswada.


Hali halisi, Halmashauri ya Chama cha Wanasheria kimeamua
kumtembelea Mtukufu Rais ili kumfikishia yeye binafsi ujumbe huu.

b. Chama kinaisihi Serikali isitafute kugundua upya gurudumu katika mchakato

huu – kwa kadiri inavyowezekana, Serikali ijifunze kutoka uzoefu wa nchi

nyingine, kama vile Kenya na Uganda.



c. Chama chetu kiko mbioni kuunda Kamati ya Katiba, ambayo- pamoja na mambo

mengine- itaishauri Halmashauri yetu juu ya maendeleo ya mchakato

unaoendeshwa na Serikali, itatoa msaada wa kitaalamu na utatoa mapendekezo

stahiki kwa Halmashauri yetu, umma na vyombo vinavyohusika na mchakato wa

kutunga Katiba.


Kama hapana budi, Halmashauri ya Chama itapanua majukumu ya Kamati hii

ili iweze kuwa msemaji kwa niaba yake kuhusu mijadala, ambayo yaweza

kuhitaji hatua zaidi.

Imewakilishwa kwa niaba ya Chama cha Mawakili Tanzania Bara

grancis K. Stolla

RAIS

No comments:

Post a Comment